Wednesday, October 14, 2015

PINDA APOKEA 205 WALIOREJESHA KADI CCM *Wamo wenyeviti nane wa vitongoji




MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambaye pia ni mjumbe
wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), Mhe. Mizengo Pinda amepokea kadi tisa
kati ya 205 zilizorejeshwa na wanachama wa CHADEMA katika kata ya
Mamba, wilaya ya Mlele kwenye jimbo la uchaguzi la Kavuu.

Ametoa kauli hiyo jana (Jumatano, Oktoba 7, 2015) wakati akizungumza
kwa nyakati tofauti na wakazi wa jimbo la Kavuu kwenye mikutano mitatu
ya hadhara iliyofanyika katika kata za Mamba, Mwamapuli na Usevya.

Mhe. Pinda alikuwa  mbunge kwenye jimbo hilo ambalo limegawanywa na
kupata majimbo matatu ya Nsimbo, Katavi na Kavuu. Wakati huo lilikuwa
likijulikana kama Jimbo moja la Katavi.

Alisema katika kipindi hiki cha kampeni, uongozi wa wilaya umepokea
wanachama 126 kutoka kata ya Chamalendi, 15 kutoka Kasansa ambao
wanane kati yao ni wenyeviti wa vitongoji, tisa kutoka Mamba na 62
kutoka Majimoto. Wanahama hao wametoka vyama vya HADEMA na ADT
WAZALENDO.

Alisema anastaafu akiwa na amani moyoni mwake kutokana na juhudi
ambazo Serikali ya awamu ya nne imezifanya kwenye mkoa wa Katavi.
“Niliamua kuacha kugombea ubunge kwa sababu ninatambua kuwa kuna watu
wengine wenye uwezo wa kuongoza,” alisema.

“Ninaondoka nikiwa nimefarijika kwa sababu Serikali imetupatia mkoa
mpya wa Katavi, tumepata wilaya tatu, halmashauri tatno na majimbo
matano ya uchaguzi. Hii itawapa fursa ya kupanga mipango yenu kupitia
madiwani wenu tofauti na zamani tulipokuwa tukisubiri kila kitu kitoke
Rukwa,” alisema.

Akizungumzia mafanikio ya serikali ya awamu ya nne, Mhe. Pinda alisema
Serikali ya CCM imekamilisha suala la mawasiliano ya simu na sasa hivi
inakamilisha suala la umeme ambao alisema hivi punde utaanza
kupatikana kwenye bonde la Rukwa.

“mwanzoni tulitaka umeme utoke Chala hadi huku bondeni lakini
kitaalamu ikabainika kwamba kadri unavyosafirishwa ndivyo unavyozidi
kupungua nguvu. Kwa hiyo. Wataalamu wameamua kuchukua umeme kutoka
Muze kuja Kasansa hadi Majimoto,” alisema huku akishangiliwa.

Alitumia fursa hiyo kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM,
Dk. John Pombe Magufuli pamoja na mgombea ubunge wa jimbo la Kavuu,
Dk. Pudensiana Kikwembe. Pia aliwanadi wagombea udiwani wa kata tisa
za jimbo hilo wakiwemo madiwani wa  kata za Mamba, Majimoto,
Mwamapuli, Ikuba, Mbede, na Kibaoni ambao walihudhuria mikutano hiyo
.

No comments:

Post a Comment