Sunday, June 21, 2015

RISALA YA WATOTO WA KAMBI YA WATOTO (ARIEL CAMP) 2015





Ndugu Mgeni rasmi,

Tunaomba kutambua uwepo wa Mkurugenzi mtendaji wa AGPAHI, Meneja wa Miradi wa AGPAHI – Shinyanga & Simiyu, wafanyakazi wa AGPAHI, Waganga Wakuu wa Mikoa ya Shinyanga na Simiyu, Madaktari kutoka Chama cha Madaktari wa Watoto Tanzania, wapendwa watoto na walezi, wageni waalikwa mabibi na mabwana.

Awali ya yote, tunachukua nafasi hii kumshukuru mwenyenzi Mungu kwa kutuamsha salama siku hii ya leo.

Tunashukuru sana ndugu Mgeni rasmi kwa kuacha shughuli zako na kukubali kuwa pamoja na sisi watoto.

Ndugu mgeni Rasmi,

Karibu katika Kambi yetu nzuri ya Ariel hapa ELCT Bukoba Hotel. Kambi hii ya Ariel ni ya tano kufanyika chini ya shirika la AGPAHI; kambi ya kwanza na ya pili zilifanyika hosteli ya Nyakahoja mkoani Mwanza, na kambi ya tatu na ya nne zilifanyika Uhuru Hotel, Mkoani Kilimanjaro. Kambi hii ya tano inafanyika hapa mkoani Kagera.

Tunapokua kwenye kambi tunapata nafasi ya kujifunza mambo mbalimbali kama vile Taarifa sahihi kuhusu VVU na UKIMWI; Ufuasi mzuri wa dawa na Kuweka wazi hali yetu; Usafi binafsi; Stadi za maisha na Mabadiliko ya tabia kutokana na msukumo wa kundi; Haki na wajibu watoto; Huduma na msaada wa kisaikolojia; Jinsia, mahusiano ya kimapenzi na Uzazi wa Mpango.


Ndugu Mgeni Rasmi
Kambi ya Ariel mwaka 2015 imefanyika hapa Bukoba, Mkoani Kagera kuanzia Jumatatu tarehe 15 Juni na tunategemea kuhitimisha baadae leo tarehe 19 Juni.

Kambi hii ya tano ya shirika la AGPAHI imetukutanisha watoto 57 kutoka Mikoa wa Shinyanga na Simiyu kwa muda wa siku tano. Watoto tuliopo hapa tuna umri wa kati ya miaka 8 hadi 17. Katika muda wa siku 5 tuliokaa hapa tumepata nafasi ya kucheza pamoja michezo mbalimbali, tumechora picha mbalimbali, tumeimba, tumecheza mpira, tumeshiriki kwenye shidano la mrembo na mtanashati wa Ariel Camp, tumepata marafiki, tumekula chakula na pia tumeelewa kuwa AGPAHI inajali watoto wakue na kuishi kwenye matumaini chanya.

Pia tumefanya matembezi na kuona mto Kagera, Kiwanda cha Sukari cha Kagera, kuona na kuelezewa maeneo ya vita vya IDD AMIN na pia tumefika kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda eneo la Mutukula.
Tumefurahi sana kwa sababu ni bahati ya aina yake tuliyoipata kupitia shirika la AGPAHI.

Ndugu Mgeni rasmi
Tunapenda kutoa shukrani zetu za pekee kwa shirika la AGPAHI kwa kubuni na kufadhili shughuli hizi za kambi ya watoto na kututhamini na kutuenzi sisi watoto. AGPAHI imetusafirisha kutoka Shinyanga na Simiyu na kutuleta hapa. Tunashukuru kwa kutujali kwa kutupa zawadi mbalimbali. Pia tunashukuru wazazi na walezi wetu kwa kuturuhusu na kutuandaa kwa safari hii yenye historia kubwa katika maisha yetu. Bila kuwasahau wenyeji wetu wa hapa ELCT Bukoba Hotel kwa mapokezi na huduma nzuri ya matunzo, chakula kizuri, malazi na mazingira tulivu.


Ombi
Ndugu Mgeni Rasmi

Tunaomba Serikali yetu iwaunge mkono shirika la AGPAHI ili huduma za kisaikolojia kwa watoto na kambi kama hizi ziendelezwe na zifikie watoto wengi zaidi kila mwaka na pia zienee Tanzania nzima.

AGPAHI inajali watoto, wakue na kuishi kwenye matumaini chanya

Risala hii imeandaliwa na watoto wa kambi ya Ariel mwaka 2015.

No comments:

Post a Comment