Monday, May 11, 2015

KESI YA MAUAJI YA ALBINO AARON NONGO YAANZA KUSIKILIZWA TENA





 KESI ya mauaji ya Aaron Nongo mwenye ulemavu wa ngozi (albino) imeanza kusikilizwa tena leo hii kwenye Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza baada ya kusimama kwa miezi takriban mitano.
 
Shauri hilo namba 213 la mwaka 2014 liko mbele ya Jaji Robert Makaramba, ambaye ndiyo kwanza ameanza kulisikiliza baada ya jaji wa awali, Ashery Sumari, kupewa uhamisho.
Washtakiwa katika kesi hiyo walikuwa watano, lakini leo hii mahakama imearifiwa kwamba mmoja – Paulo Budeba Genji maarufu kama Lumalija – alifariki dunia Novemba 22, 2014 katika Hospitali ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure, wakati akiwa mahabusu.

Taarifa hiyo ilitolewa na kiongozi wa mawakili wa upande wa mashtaka, Emil Kiria, ambaye aliiomba mahakama, akirejea Kifungu cha 284 (a) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, kwamba inapotokea hali kama hiyo mashtaka dhidi ya mtu huyo yanafikia kikomo, ombi ambalo lilikubaliwa na mahakama.

Washtakiwa waliobakia kwenye kesi hiyo ni Chacha Jeremia, Mathew Jeremia Mlimi, Paschal Lugoye Mashiku na Alex Joseph maarufu kama Bugwema Silola Jangalu.
Kesi hiyo ambayo inaendelea tena kesho katika Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, iko katika hatua ya ushahidi ambapo shahidi wa sita wa upande wa mashtaka atatoa ushahidi wake.

Leo hii mashahidi wawili wametoa ushahidi wao na kufanya idadi ya mashahidi waliokwishatoa ushahidi wao kufikia watano mpaka sasa.
Marehemu Nongo aliuawa Juni 26, 2009 majira ya saa tatu usiku akiwa nyumbani kwake Ibanda Relini, jijini Mwanza ambapo wauaji hao walimkata usoni na kisha kumkata miguu yake yote miwili na kutoweka nayo pamoja na meno mawili ya mbele.
 

No comments:

Post a Comment