Friday, March 28, 2014

MRADI WA DASIP WATOA ZANA ZA KILIMO NA VITENDEA KAZI VINGINE

 Moja ya vifaa vilivyotolewa na mradi wa uendelezaji kilimo nchini (DASIP), hiki ni kifaa cha kupanda mpunga.

 Mkuu wa mkoa wa Kagera Kanali mstaafu Fabian Massawe akiwasha moja ya zana za kilimo zilizotolewa na mradi wa DASIP.


Serikali  inaendelea kuboresha na kuimarisha kilimo kwa wananchi wa mkoa wa Kagera kwa kutoa vifaa vya kisasa vya kilimo kupitia mradi wa uwekezaji katika sekta ya kilimo Wilayani (District Agricultural Sector Investment Project – DASIP)
Serikali kupitia Mradi wa DASIP imetoa zana za kisasa za  kilimo na vifaa mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza kilimo cha kisasa na chenye tija katika Halmashauri saba za Wilaya za Mkoa wa Kagera ili ziweze kuinua uchumi wa wananchi wake kupitia kilimo cha kisasa.
Zana na vifaa vilivyotolewa na serikali kupitia mradi wa DASIP mkoani  Kagera ni  matrekta madogo (Powertllers)manne, Mashine za kupandia mpunga (Transplanters) 4, Kasiki (Cash boxes) 18 za kutunzia fedha kwenye SACCOS vijijini, na Kompyuta 6 kwaajili yakutunzia kumbukumbu za kilimo za wakulima.
Gharama ya zana na vifaa hivyo vya kilimo kwa jumla ni shilingi milioni 174,000,000/= vikiwa na mchangunuo ufuatao, trekta ndogo 4 za kilimo kila moja sh 5,000,000/=, Mashine za kupandia mpunga 4  kila moja sh 13,000,000/=, Kompyuta 6 kila moja sh 2,000,000/= na kasiki 18 kila moja sh 500,000/=.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe Massawe akikabidhi zana na vifaa vya  kilimo kwa Wakurugenzi watendaji wa halmashauri  aliishukuru serikali kutoa zana hizo za kisasa ambazo zitawafanya wakulima wa mkoa waKagera  kuzalisha kwa wingi mazao ya chakula na biashara  kwa wakati muafaka.
Aidha kutokana na mradi wa DASIP kuonyesha mafanikio makubwa mkoani Kagera Mhe. Massawe aliiomba serikali kuongeza muda wa mradi huo ambao ulianza mwaka 2006 na kumaliza muda wake mwezi desemba 2013.
“Kama ilivyo miradi mingine mfano TASAF naiomba serikali kuongeza muda wa mradi huu wa DASIP au serikali ifikirie kuanza DASIP II ili kunufaisha wananchi walio wengi mkoani kwetu Kagera kwani mradi huu umekuwa wa tija kwa wakulima wetu,” Alitoa wito Mhe Massawe.
Katika hatua nyingine Mhe. Massawe aliwaasa Wakurugenzi kuhakikisha zana hizo zinakwenda kwa wakulima walengwa ili wazitumie na kuzifanya halmashauri za wilaya kujiongezea mapato ya ndani kupitia kilimo.
Lengo la mradi wa DASIPlilikuwa ni kuchangia katika kupunguza umasikini vijijini kwa kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo hatimae kuongeza patola mkulima na uhakika wa chakula katika kaya, aidha, DASIP ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa kuendeleza sekta na mipango ya kilimo.
Mradi wa DASIP ulikuwa unafanya kazi katika sehemu kuu nne ambazo ni Uimarishaji wa uwezo wa wakulima,  Uandaaji wa mipango ya maendeleo ya kilimo na uwekezaji katika kilimo, Uimarishaji wa vyama vya kuweka na kukopa pamoja na masoko na mwisho ni Uratibu wa mradi wenyewe.

Halmashauri za Wialaya za mkoa wa Kagera zilizonufaika na vifaa vya kilimo kutoka katika mradi wa  DASIP ni Bukoba, Biharamulo, Chato (Mkoa mpya wa Geita), Karagwe, Missenyi, Muleba na Ngara.  Aidha, halmashauri hizo zimeingiza miradi ya DASIP katika bajeti za kila mwaka ili kuhakikisha shughuli zote zilizokuwa zikifanywa na DASIP zinaendelea na kwa ufanisi mkubwa.

No comments:

Post a Comment