Thursday, November 07, 2013

Kikwete:Tanzania haitajitoa A.Mashariki


Tanzania imesema hataitajitoa katika Jumuiya ya Afrika kama wengi walivyodhani na badala yake imedhamiria kuhakikisha Jumuiya hiyo inadumu na kustawi.
Akilihutubia bunge la Tanzania, mjini Dodoma, katikati mwa Tanzania, Rais wa nchi hiyo, Jakaya Kikwete amesema kwamba Tanzania haina mpango wala fikra za kujitoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kuwa ni nchi inayoamini katika umoja na maendeleo na imekuwa ikitumia gharama kubwa kuhakikisha jumuiya hiyo inaimarika.
"Tanzania ni mwanachama mvumilivu, mtiifu na mwaminifu na tunatimiza wajibu wetu kwa jumuiya na kuhusika kikamilifu katika ujenzi wake." amesema Rais Kikwete.
Rais Kikwete ametumia muda mrefu katika hotuba hiyo kuchambua masuala mbalimbali ya msingi ya uhai wa jumuiya hiyo huku akisema ameshangazwa na nchi za Kenya, Uganda na Rwanda kuzitenga Tanzania na Burundi.
Amesema kuna masuala ambayo hayazifungi nchi wanachama katika mkataba wa umoja wao, hivyo kuwa na uhuru wa ushirikiano na nchi ndani ya jumuiya na hata nje.
"Naomba kwanza niweke wazi jambo moja, kwamba nchi mbili wanachama au zaidi hazikatazwi kuwa na makubaliano ya ushirikiano katika kufanya mambo mbalimbali. Hata sisi Tanzania tunao ushirikiano wa namna hiyo na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Lakini, nchi wanachama zinatakiwa kufanya hivyo kwa yale mambo ambayo hayako kwenye shughuli za Jumuiya kwa maana kwamba hayamo katika Mkataba au Itifaki au hakuna uamuzi wa msingi uliofanywa na vikao au taasisi za Jumuiya kuyashughulikia. Pia, tunaweza kufanya hivyo kwa mambo ambayo yalishaamuliwa na Jumuiya yatekelezwe na ruhusa imetolewa kwa nchi yo yote iliyokuwa tayari kutekeleza ama peke yake au kwa kushirikiana na nchi nyingine".
Hata hivyo Rais Kikwete amesema huenda mambo yanayoitenga Tanzania na nchi nyingine tatu za jumuiya ya Afrika Mashariki, ni msimamo wake kuhusu kuharakisha shirikisho, masuala ya ardhi, ajira, na uhamiaji.
Pia Rais Kikwete amesema Tanzania haina mpango wa kujitoa kwa kuwa inaamini na ina uhakika kuwa haijafanya jambo lolote baya dhidi ya jumuiya au nchi mwanachama yeyote wa jumuiya hiyo.

No comments:

Post a Comment