Thursday, August 15, 2013

KAMATI YA BUNGE YA MIUNDO MBINU MKOANI KAGERA



Kamati ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania ya Miundombinu  ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Peter Joseph Serukamba (Mbunge Kigoma Mjini) ilifanya ziara ya kukagua miundombinu ya bandari na viwanja vya ndege mkoani Kagera  jana  Agosti 14, 2013.
Kamati hiyo mara baada ya kuwasili mkoani Kagera  na kupokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera ofisini kwake majira ya saa 5:00 asubuhi  ilianza ziara yake mkoani hapa kwa kutembelea bandari za Bukoba na Kemondo kujionea miundombinu ya bandari hizo.
Katika bandari ya Bukoba baada ya  kutembelewa na kukaguliwa Kamati  iliuagiza  uongozi wa bandari kufanya ukarabati wa haraka katika sehemu ya abiria kwa kufumua paa ambao limezeeka na kullipandisha juu zaidi ili kuruhusu hewa zaidi katika eneo hilo na kweka paa jipya lisilovuja.
Pia katika Bandari ya Kemondo Mwenyekiti wa kamati Mhe. Serukamba baada ya kusomewa taarifa  alimwagiza Katibu Mkuu Wizara ya  Uchukuzi kuhakikisha mara moja nyumba za watumishi zilizoko katika eneo la bandari ya Kemondo zilizochukuliwa  na Shirika la nyumba la Taifa zinarejeshwa kwa mmiliki wake wa awali ambaye ni bandari ya Kemondo.
Katika hatua nyingine wajumbe wa Kamati walitembelea Wilayani Missenyi na kukagua eneo la Omukajunguti ambapo serikali inatarajia kujenga uwanja wa kimataifa wa ndege. Katika eneo hilo Kamati ilitoa maelekezo kwa taasisi inayohusika, Wizara na Halmashauri kukamilisha maandalizi ya kiwanja hicho.
Kamati iliagiza Wizara ya Uchukuzi kushirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (TIAA) pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi kukaa pamoja na kuweka mipaka halisi ya kiwanja cha Omukajunguti pia kufanya tathimini na kuwalipa wananchi fidia zao ili kupisha ujenzi wa uwanja huo.
Aidha katika Uwanja wa Ndege wa Bukoba wajumbe wa Kamati waliridhika na maendeleo ya ujenzi na kumsisitiza Mkandarasi kuhakikisha anamaliza kazi zake kwa muda aliopewa kufikia Februari 2014. Aidha Wizara kuhakikisha inawalipa fidia wananchi ambao bado hawajalipwa fidia zao kiasi cha milioni 900 katika mwaka huu wa fedha 2013/2014.
Gari la Wabunge Lapata Ajali
Wakati msafara wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu ukielekea Wilayani Missenyi kukagua sehemu utakapojengwa  uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Omukajunguti, gari aina ya Costa lenye namba za usajili T 570 BYU lilowabeba Waheshimiwa Wabunge 11 lilipata hitirafu na kutaka kuungua.
Ajali hiyo ilitokea eneo la Mwanzo Mgumu kilometa moja kutoka mpakani mwa Wilaya ya Bukoba na Wilaya ya Missenyi ambapo gari hilo aina ya costa lilianza kutoa moshi mwingi kwa upande wa nyuma wakati likiwa kwenye mwendo mkali na kuleta hofu kubwa kwa abiria walikuwemo ndani ya gari hilo.
Mara baada ya dereva wa costa kugundua kuwa gari linataka kuungua alifanikiwa kulisimamisha gari hilo na kuwaambia abiria wake kuwa gari linaungua na alitoka haraka ndani ya gari na kutimua mbio na kuwaacha wabunge wakiangaika kutoka wakati gari likitoa moshi mwingi sana.
Kwa mujibu wa wabunge walikuwemo kwenye gari hilo walisimulia kuwa baada ya kuambiwa kuwa gari linaungua kila mmoja alifanya juhudi za kujiokoa yeye mwenyewe ambapo mmoja wao alipita dirishani na wengine walifanikiwa kusukuma mlango na  ukafunguka na kutoka salama.
Kwa Bahati hakuna Mbunge aliyeumia isipokuwa Mhe. Batenga  aliumia mkono kidogo baada ya kubanana sana mlangoni. Baada ya kila mmoja kutoka gari hilo liliendelea kutoa moshi mzito sana lakini kwa  halikushika moto na baadae lilizika na kuacha kutoa moshi.
Wabunge waliokuwemo katika gari hilo ni Rebbecca Mngondo (Arusha Viti Maalumu), Rita Kabati (Iringa Viti Maalumu), Mariam Msabaha (Zanzibar Viti Maalumu), Mhe. Batenga (Kagera Viti Maalumu), Mhe. Madabida (Dar es Salaam Viti Maalum), Clara Mwatuka (Mtwara  Viti Maalumu).
Wengine ni Mzee Hussein (Zanzibar), Mussa Haji Kombo (Pemba Zanzibar), Abdul Mteketa (Jimbo la Kilombelo), Mutula Mutula (Jimbo la Tunduru Kusini). Aidha Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Peter Serukamba Hakuwemo katika gari hilo lilotaka kuungua.
Imeandaliwa na:
Sylvester Raphael
AFISA HABARI
RS-KAGERA@2013

No comments:

Post a Comment