Tuesday, June 04, 2013

SABABU ZA VIFO VILIVYOTOKANA NA MLIPUO WA UGONJWA WA MALARIA ZAELEZWA

 
ZAIDI ya watu 23 wamekufa wilayani Muleba kufuatia kuzuka kwa mlipuko wa ugonjwa malaria ambao ni pamoja watoto 16 chini ya umri wa miaka 5 na watu wazima 7 kati ya mei 20 hadi mei 31, mwaka huu.
 
Kwa mujibu wa taarifa ambazo gazeti hili lilizipata na ambazo zilithibitishwa na mkuu wa wilaya ya Muleba, Lembres Kipuyo jana ni kwamba vifo hivyo vilitokea katika hospitali teule ya wilaya hiyo ya Rubya.
 
 
Alisema katika wilaya hiyo maeneo ambayo yamekubwa na mlipuko wa ugonjwa wa Malaria kuwa ni yale ya vijiji vinavyozuka mto Ngono ambao maji yake hutiririka hadi Wilayani Missenyi.
 
Mkuu huyo wa wilaya alisema vifo vingi vilichangiwa na uhaba wa madawa, alisema baada ya mlipuko wa ugonjwa huo kutokea hospitali teuli ya Rubya ilikuwa na kiasi kidogo cha madawa ya kutibu ugonjwa wa Malaria.
 
 
 
uongozi wa  wilaya hiyo kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa umeunda mikakati madhubuti ya kudhibiti ugonjwa huo ambayo ni pamoja namna ya kupata madawa kwa ajili ya kudhibiti mlipuko huo ambao ni tishio kwa maisha ya watu.
 
 
Amesema hatu nyingine ambayo uongozi wa wilaya ya Muleba umeichukua ya kudhibiti ugonjwa huo ni pamoja na kuwahamasisha wananchi wanaoishi kwenye maeneo mlipuko wa malaria ulipojitokeza kuyafanyia usafi maeneo yao ili waue mazalia ya mbu wanaoeneza malaria.
 
 
Hata hivyo pamoja na jitihada za uongozi wa wilaya ya Muleba kufanya za kuthibiti mlipuko huo, baadhi ya wananchi ambao hawakutaka majina yao yatajwe waliliambia gazeti hili kuwa vifo vya watu vilivyotokana na mlipuko wa ugonjwa wa malaria kuwa vilichangiwa na uongozi wa wilaya hiyo.
 
Wakiongea kwa nyakati tofauti waliliambia gazeti hili kuwa baada mlipuko kujitokeza viongozi walikuwa na taarifa lakini hawakuchukua hatua za haraka za kuthibiti hali hiyo hadi wananchi walipoanza kueleza kilio chao ndipo viongozi walishtuka, walisema ndio maana wagonjwa waliopelekwa Rubya kwa matibabu walikosa msaada wa haraka ambao ni pamoja na madawa.
 
 
Walisema wananchi walipokuwa wakifikishwa hospitalini walikuwa wakilazwa katika hospitali ya Rubya bila msaada wowote, waliendelea kusema kuwa hali hiyo ndio ilichangia vifo vya watu wengi, walisema wagonjwa walikuwa wakipewa maji tu.  
 
 
Walidai kuwa kama uongozi wa wilaya ya Muleba kama ungechukua hatua za haraka za kuthibiti mlipuko wa ugonjwa huo kwa kusambaza madawa ya malaria kwa wakati vifo vingepungua sana.
 
 
"Ndugu waandishi msidanganywe hata waliolazwa afya mawodini mkiwaona afya zao sio nzuri uko uwezekano wa kutokea vifo vingine vingi zaidi, hali ni mbaya sana, muandike taarifa sahihi msipotoshwe na baadhi wa viongozi wanaotaka kufagilia unga wao" alisema mmoja wa wananchi.
 
"Hapa viongozi hasa wa halmashauri ya wilaya ya Muleba wanapaswa kuwajibika kwa suala hili, mimi binafsi naiomba serikali ichukue suala hili kwa umakini zaidi kwa kuwa wameonyesha uwajibikaji mdogo" alisema mwananchi mwingine bila kutaja jina lake.
 
Kufuatia kuzuka kwa mlipuko wa ugonjwa huo katika Hospitali ya Rubya imefurika wagonjwa kiasi cha uongozi wa hospitali kulazimika kuwalaza mgonjwa zaidi ya watatu  kwenye kitanda kimoja.
 
Katika hatua kuwafariji wanaougua ugonjwa wa Malaria waziri ardhi nyumba na maendeleo ya makazi, Profesa Anna Tibaijuka, ametoa msaada wa vyakula vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 1.5.
 
Msaada ulitolewa na Profesa Tibaijuka ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Muleba kusini  ulikabidhiwa na katibu wake wa jimbo hilo la Muleba Kusini, Denis Mutajwaha alipofika katika hospitali ya Rubya kuwafariji wagonjwa.
 
 
 
Hii ni mara ya pili mlipuko wa ugonjwa wa Malaria kuzuka wilayani Muleba, tabribani zaidi ya miaka 5 iliyopita mlipuko wa ugonjwa huo ulijitokeza na kusababisha vifo vya watu wengi.
 

No comments:

Post a Comment